Sunday 24 January 2016

WAFANYAKAZI WA NDANI..

Nimekuwa naletewa maswali ambayo yamekuwa yakinipa picha tofauti kuhusu wafanyakazi wa ndani (house maids) hasa kwa wanawake kulalamikia waume zao au ndugu zao wa kiume kutembea na wafanyakazi wao wa ndani wa kike (house girls) na pia wanaume kulalamika kwamba wake zao hutembea na wafanyakazi wao wa ndani wa kiume (house boy)
Je, ni kweli kwamba hawa wafanyakazi ni hatari kwa ndoa zetu pia kama wanandoa wanakuwa hawapo makini?
Baada ya kupita mtaani na kuwauliza baadhi ya akina mama walikuwa na haya ya kuchangia na swali lilikuwa:-
Je, Ungependa kuwa na mfanyakazi wa nyumbani mvulana( house boy) au msichana (house girl)?

MAJIBU..
Binafsi napenda mfanyakazi wa ndani ambaye ni msichana kutokana na kazi ya kutunza mtoto na pia kwa usalama kwani ni rahisi kumthibiti msichana kuliko mvulana.
Wasichana ni wazuri zaidi kwa masuala ya ndani ingawa nitakuwa makini kumbadilisha kabla hajaanza kufanya vitu vyake
Dina – Kawe Dar es Salaam
Mimi nitapenda kuwa na mfanyakazi wa ndani mvulana tena awe na umri wa miaka 13 hadi 16 kwani mvulana wa umri huu hawezi kuleta kasheshe ukilinganisha na wasichana wa siku hizi. Pia kuwa na mfanyakazi wa ndani msichana ni kama kuweka tangazo kwamba mume wako sasa amepata mke mwingine.
Leo maadili yameshuka sana na hawa mabinti ni hatari sana na wanaweza kufanyia lolote kuhakikisha ndoa yako inaweza kuwa tofauti kukiwa na hiyo nafasi.
Nimeshuhudia msichana wa kazi wa miaka 20 akisababisha mama mwenye nyumba kuachana na mume wake na yeye kuchukua usukani hivihivi. Hii ina maaa wasichana wa kazi wa leo wanahitaji usimamizi mkali sana hasa kutokuwa na nafasi ya kuingia chumbani hasa ukiwa hupo nyumbani na mume akiwa nyumbani peke yake na huyo binti.
Mama junior – Ilala Dar es Salaam

Mimi napenda kuwa na mfanyakazi wa kiume kwani wapo imara na hakuna longolongo kazi ni kazi, mabinti sana sana itakuwa ni kukuzunguka ili mume wako anaswe na hata kukuibia mali zako na wakati mwingine kiburi na hata kuhakikisha mambo yako hapo nyumbani hayaendi na kukufanya mume akuone hufai na yeye anafaa na unajua nini kitafuata....
Jane – Kimara Dar es Salam
Naona hapa inabidi kuwa makini, binafsi kama nitakuwa na msichana wa kazi jambo la msingi ni kuhakikisha umri wake si zaidi ya miaka 14 kwani ukiwa na msichana wa kazi ambaye ameshakua (mature) hapo unacheza na ndoa yako kwani wanaume hushawishika na kile wanaoana, wapo dhaifu sana wanapoona mabinti wanaojiremba siku hizi (matiti na mwili nusu uchi) na huyo house girl anaweza kumjaribu mume wako na anaweza kufanyia kile ambacho hakuwa nacho akilini.
Ukweli usipokuwa makini na haya mambo unaweza kujuta.
Pia sidhani kuna kitu kitaweza kunizuia kuwa na mfanyakazi mvulana hata hivyo lazima awe mvulana mdogo na si mwanaume mtu mzima kwani tumesikia wengine wameishia kubaka, kuwapa mimba wanafamilia wa kike na hata kuiba mali na kuondoka nazo, Ukweli hawa wanaume wanaopewa kazi za kufanyia ndani ya nyumba zetu ni hatari zaidi kuliko mabinti.
Mama Jenifer – Magomeni Dar es Salaam


Kwa ushauri wangu nitapenda kuwa na mfanyakazi wa ndani mwanaume kwa kuwa wao ni hodari na wapo rahisi kuliko wasichana.
Pia kama ni mwanamke ukisafiri huna wasiwasi kwa kuwa wanakuwa makini na kazi zao na si sawa na mabinti ambao unaondoka huku nyumba hujui mume wako itakuwaje na hao wasichana ambao siku hizi ni homa ya jiji.
Joyce mgaya – Sinza Dar es Salaam

Kwa upande wangu nitapenda kuwa na msichana chini ya miaka 11 kwani yeye ana upendo wa mama kwa watoto wangu na pia kazi za ndani kitu kimoja ambacho lazima niweke wazi ni kwamba hataruhusiwa kufua nguo za mume wangu au kwenda chumbani Kwangu na mume wangu.
Mvulana hapa kwani nina mabinti nyumbani na anaweza kuleta shughuli nzito kwa mabinti zangu na nikajuta.
Mama Yuster Kimara Dar es Salaam

Kwa upande wangu sihitaji mfanyakazi yeyote awe msichana au mvulana kwani mabinti zangu ni wakubwa sasa na pia naziweza kazi zangu zote za hapa nyumbani na hata kama ni nyingi watoto wangu hunisaidia.
Mama James Mbezi Dar es Salaam

Mimi nitatafuta mwanamke mtu mzima ambaye anaweza kufanyia kazi na atakuwa anafanya kazi na kurudi kwake, siwezi kuchukua wasichana wadogo ambao wamekua tayari kwani napenda mume wangu abaki wangu mwenyewe na si vinginevyo.
Mama Helena – Kimara Dar es Salaam
Je, wewe unasemaje

No comments:

Post a Comment