Thursday 10 March 2016

EPUKA KUTUMIA NENO HILI..

Naomba jiulize kidogo hivi ni mara ngapi kunapotokea mgogoro katika ndoa yako umekuwa unawaza au kutishia kwamba utaachana na huyo mume wako au mke wako?

Inawezekana unaishi katika wakati mgumu sana katika ndoa yako umeumizwa sana, umekatishwa tamaa sana, hupendwi, hakujali tena, umejawa na stress kiasi kwamba hata unapotamka kwamba afadhari kupata talaka na kujianzia maisha mapya kivyako huoni uzito wa neno talaka unavyolitamka.
Ukweli ni kwamba kwa maneno yetu tunayotamka tunaweza kuweka mustakabali wa maisha yetu ya baadae.
Maneno hushibisha nafsi sawa na chakula



Maneno tunayoongea yana uwezo wa ajabu ndani yake; yana uwezo kuponya au kuua au kuumiza, yana uwezo wa kutia moyo au kukatisha tamaa kabisa, yana uwezo wa kusema ukweli au kudanganya kwa uwongo wa ajabu, yanauwezo kutoa sifa au kulaumu, yana uwezo wa kubariki au kulaani nk.

Neno talaka ni neno lenye sumu na neno baya sana kulitumia katika ndoa yako na zaidi ya yote huweza kuumba kwenye akili na mawazo yako zaidi ya wewe unavyofikiria na kutoa matokeo sawa na mbegu iliyopandwa.

Unapotamka maneno mabaya kwa ndoa yako au katika maisha yako ya kila siku unamwaga sumu na ipo siku itakuwa kweli kwani kila unachopanda lazima utavuna.

Kawaida maneno tunayoongea kwenye ndoa zetu ni kama kioo kwa mwingine (mwanandoa mwenzako).
Ukisema nakupenda, mwenzako anajisikia vizuri na kujihisi kweli anapendwa;
Ukisema umependeza, atajisikia vizuri na kujiona amependeza;
Ukisema ndoa chungu, na mwenzako atajisikia ndoa chungu,
Ukisema nitakufa ni kweli utakufa kabla ya muda wako.

Hivyo ni vizuri kila mmoja kuongea maneno yanayojenga ambayo ni positive ili ndoa zetu zidumu.
Ukizoea kutamka neno talaka ni kweli usishangae siku ndoa inaishia kule unaitamkia hata kama ulikuwa unatania.
Ndoa haitaniwi!
Neno talaka inabidi lifutwe kwenye misamiati yako hasa baada ya kuoa au kuolewa

Duniani tuna watu wa aina tatu tu:
Kwanza wale wanafikiri chakuongea kabla ya kuongea
Pili wale wanafikiri cha kuongea huku wanaongea
Tatu wale wanaongea kwanza ndo wanafikiria nini wameongea
Wewe upo kundi gani na unatumia vipi uwezo wako wa maneno?

No comments:

Post a Comment